Friday, July 31, 2015

FENERBAHCE YAIKATIA RUFANI SHAKHTAR KWA KUMCHEZESHA FRED.

KLABU ya Fenerbahce imetuma malalamiko yake Shirikisho la Soka la Ulaya-UEFA baada ya Shakhtar Donetsk kumchezesha kiungo wa kimataifa wa Brazil Fred dhidi yao, pamoja na kukabiliwa na tuhuma za kutumia dawa za kusisimua misuli. UEFA imethibitisha kuwa inafanyia uchunguzi mchezo huo wa mkondo wa kwanza wa hatua ya tatu ya kufuzu michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya uliochezwa Jumanne iliyopita na kumalizika kwa sare ya mabao 2-2. Taarifa kutoka nchini Brazil zinadai kuwa Fred mwenye umri wa miaka 22, alikutwa na chembechembe za dawa hizo zilizopigwa marufuku wakati alipofanyiwa vipimo katika michuano ya Copa America iliyomalizika hivi karibuni huko Chile. Kocha wa Shakhtar Mircea Lucescu amekiri UEFA walimshauri kutomchezesha Fred katika mchezo huo. Mchezaji huyo atakabiliwa na adhabu ya kufungiwa kama vipimo vya pili vitathibitisha kuwa alitumia dawa hizo.

No comments:

Post a Comment