Sunday, March 31, 2013

Top 100 Goals of the Year 2012

FIFA YAIONYA AFRIKA KUSINI.

SHIRIKISHO la Soka Duniani-FIFA limeiandikia barua serikali ya Afrika Kusini kuwaonya kufanya uchunguzi wa kimahakama juu ya kashfa ya upangaji matokeo wakidai kuwa suala hilo ni bora likashughulikiwa na Chama cha Soka cha nchi hiyo-SAFA. Mechi kadhaa za Afrika Kusini walizocheza kabla ya michuano ya Kombe la Dunia 2010 zimegundulika kwamba zilipangwa na kupelekea baadhi ya viongozi wa juu wa SAFA kusimamishwa akiwemo rais wake Kirsten Nematandani. Shirikisho la Michezo nchini humo pamoja na Kamai ya Olimpiki wamependekeza kufanyika uchunguzi wa kimahakama lakini FIFA waliwaonya juu ya madhara yanayoweza kuwakuta kama serikali itaonekana kuingilia masuala ya soka. Waziri wa Michezo wa Afrika Kusini, Fikile Mbalula aliviambia vyombo vya habari vya nchi hiyo kuwa atasafiri kwenda makao makuu ya FIFA jijini Zurich wiki ijayo kwa ajili kuzungumzia suala hilo.

O'NEILL ATIMULIWA SUNGERLAND.

KLABU ya Sunderland ambayo iko kwenye hatari ya kushuka daraja imemtimua meneja wake Martin O’Neill kufuatiwa matokeo mabaya ambayo imekuwa ikipata timu hiyo. Sunderland ambao wanajulikana kwa jina maarufu la paka weusi wako alama moja juu ya msatari wa kushuka daraja huku wakiwa wamebakiwa na michezo saba baada ya kufungwa na Manchester United Jumamosi. Klabu hiyo imesema wameamua kuvunja mkataba na O’Neill na kumshukuru kocha huyo katika kipindi chote alichokuwepo hapo pia kumtakia kila la kheri huko aendapo. Pia klabu hiyo imedai itatangaza mbadala wa O’Neill katika chache zijazo. Kuondoka kwa O’Neill kunafikisha idadi ya mameneja watano wa Ligi Kuu nchini Uingereza waliopoteza vibarua vyao wengine wakiwa ni Roberto Di Matteo wa Chelsea, Mark Hughes wa Queens Park Rangers, Nigel Adkins wa Southmpton na Brian MarkDermott wa Reading.

SERENA AWEKA REKODI MICHUANO YA SONY OPEN.

MCHEZA tenisi namba moja katika orodha za ubora duniani kwa upande wa wanawake, Serena Williams amefanikiwa kushinda michuano ya wazi ya Sony baada ya kumfunga Maria Sharapova kwa 4-6 6-3 6-0 na kuweka rekodi ya kunyakuwa taji hilo mara sita. Williams ambaye amefikia rekodi ya nyota wa zamani wa tenisi Steffi Graf ambaye naye amewahi kunyakuwa michuano hiyo ya Miami mara sita. Williams ambaye ni raia wa Marekani amefanikiwa kushinda taji hilo mwaka 2002, 2003, 2004, 2007 na 2008 huku akimaliza katika nafasi ya pili mwaka 1999 na 2009. Akihojiwa mara baada ya mchezo huo Williams amesema kushinda yaji hilo ni kitu ambacho hakukitegemea wakati mashindano hayo yanaanza lakini anashukuru amepambana mpaka kuhakikisha ananyakuwa taji hilo kwa mara ya sita.

MISRI WATAWAZWA MABINGWA WAPYA WA MICHUANO YA U20 AFRIKA.

TIMU ya taifa ya vijana chini ya miaka 20 ya Misri jana wametawadhwa mabingwa wapya wa michuano ya Afrika kwa vijana wa umri huo baada ya kuifunga Ghana kwa changamoto ya mikwaju ya penati 5-4 baada ya kutoka sare kwa kufungana bao 1-1 katika muda wa kawaida. Vijana hao wa Misri ambao wanajulikana kama The Young Pharoahs yaani Mafarao Wadogo hili linakuwa taji lao la nne kwa michuano hiyo wakiizidi Ghana kwa taji moja baada ya ya kulinyakuwa mara tatu. Katika mchezo huo Misri ndio walikuwa wa kwanza kupata bao katika dakika ya ya nne kwa njia ya penati baada ya Saleh Gomaa kuangushwa katika eneo la hatari lakini iliwachukua Ghana dakika tatu kurudisha bao hilo baada ya wao pia kupata penati iliyofungwa na Jeemiah Arkoful. Baada ya kufungwa mabao hayo timu zte ziliendelea kushambuliana kwa zamu lakini mpaka mpira unamalizika na kuongezwa dakika 30 hakuna timu iliyoweza kuona lango la mwenzake hivyo kupelekea kupigiana matuta.

MESSI AWEKA REKODI NYINGINE.

MSHAMBULIAJI nyota wa Barcelona, Lionel Messi amefanikiwa kufunga bao katika mechi 19 mfululizo za Ligi nchini Hispania na kuweka rekodi mpya kwa kuifunga kila timu walioyokutana nayo katika ligi hiyo msimu huu. Mshambuliaji huyo wa kimataifa kutoka Argentina alitengeneza bao la kwanza na kufunga la pili lakini Celta Vigo ambao wanapambana wasishuke daraja walifanikiwa kusawazisha bao hilo katika dakika ya 88 na kupelekea mchezo huo kumalizika kwa sare ya mabao 2-2. Hilo linakuwa bao lake la 30 katika mechi 19 ambapo sasa amefikisha jumla ya mabao 43 katika mechi 29 walizocheza msimu huu na kubakisha mabao saba kufikia rekodi ya mabao 50 aliyoweka msimu uliopita huku kukiwa kumebakia mechi tisa. Messi ambaye kwa mara ya kwanza katika mchezo alikuwa nahodha amesema anashukuru kwakuwa amekuwa na bahati ya kufunga na kuisaidia timu na huwa hatilii maanani rekodi anazovunja cha muhimu ni timu yake kushinda.

Saturday, March 30, 2013

MURRAY, FERRER KUCHUANA FAINALI SONY OPEN.

MCHEZA tenisi nyota kutoka Uingereza, Andy Murray amefanikiwa kuingia hatua ya fainali ya michuano ya wazi ya Sony baada ya kumfunga Richard Gasquet wa Ufaransa kwa 6-7 6-1 6-2. Katika mchezo huo Murray ilibidi apigane kufa na kupona baada ya kupoteza seti ya kwa Gasquet ambaye alionekana kuwa katika kiwangi kizuri katika mchezo huo. Fainali ya michuano hiyo ambayo inafanyika jijini Miami, Florida inatarajiwa kutimua vumbi kesho ambapo Murray atachuana na David Ferrer wa Hispania. Akihojiwa mara baada ya mchezo huo Murray amesema mpinzani wake alimpa wakati mgumu kwenye mchezo huo hususani katika seti ya kwanza lakini anashukuru alirekebisha makosa aliyofanya na kuhakikisha anaibuka mshindi kwenye mchezo huo.

NYOTA WATATU WA DC MOTEMA WAFA KWA AJALI.

WACHEZAJI watatu wa klabu ya DC Motema pembe-DCMP ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo-DRC wamefariki dunia kwa ajali ya gari iliyotokea jijini Kinshasa jana. Wachezaji hao ambao ni golikipa Guelor Dibulana, washambuliaji Hugues Muyenge na Mozart Mwanza walikuwa wakirejea kutoka katika maombi katika kanisa la Saint- Dominique lililopo Kinshasa ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya sikukuu ya Pasaka ambapo gari lao liligongwa na lori. Kwa mujibu wa taarifa za hospitali mchezaji mwenzao Mbindi ambaye alikuwa akiendesha gari hilo alisalimika pamoja na abiria mwingine lakini wote walipata majeraha makubwa. DCMP ilitarajiwa kupambana na AS Vita Club siku ya Jumapili ya Pasaka na haijajulikana kama ratiba hiyo itaahirishwa kutokana na tukio hilo la kuhuzunisha lililotokea.

FIFA YAIPA TOGO DOLA 850,000.

SHIRIKISHO la Soka Duniani-FIFA limeitoa kiasi cha dola 850,000 kwa Shirikisho la Soka nchini Togo-TFF kwa ajili ya miradi ya maendeleo kwa mwaka 2013 na 2014. Wawakilishi kutoka FIFA na Shirikisho la Soka barani Afrika-CAF walitembelea taifa hilo lililopo magharibi mwa Afrika jana na kutangaza kutoa kiasi hicho katika mkutano na vyombo vya habari. Mkuu wa kitengo cha mpango wa maendeleo wa FIFA, Cyril Loisel amesema sehemu ya fedha hizo zitatumika kwa ajili ya kuboresha michuano ya ligi daraja la kwanza na pili nchini humo. Ujumbe huo wa FIFA na CAF pia ulizungumza na viongozi wa TFF kuangalia uwezekano wa kuanzisha ligi ya soka ya wanawake nchini humo ili kuinua soka lao.

VILANOVA AANZA KIBARUA.

MENEJA wa klabu ya Barcelona, Tito Vilanova anaweza kurejea katika benchi la ufundi wiki ijayo wakati timu yake itakapochuana na Paris Saint Germain katika mchezo wa kwanza war obo fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Mapema wiki hii Vilanova alirejea nchini Hispania bada ya kupatiwa matibabu ya kansa kwa miezi miwili jijini New York, Marekani. Kocha huyo mwenye umri wa miaka 44 ambaye alichukua mikoba ya kuinoa timu hiyo kutoka kwa Pep Guardiola mwanzoni mwa msimu huu alirejea katika mazoezi ya klabu hiyo lakini alishauriwa kutosafiri na timu hiyo katika mchezo wa leo wa La Liga dhidi ya Celta Vigo. Kwa upande mwingine beki wa kimataifa wa Ufaransa na Barcelona, Eric Abidal ametajwa katika kikosi kitakachocheza na Celta Vigo baada ya kupita mwaka mmoja baada ya kufanyiwa upasuaji wa kupandikiza ini lingine. Abidal mwenye umri wa miaka 33 alifanyiwa upasuaji huo mwaka jana baada ya uvimbe uliogundulika kwenye ini lake Machi 2011 kurejea tena.

BOLT KUREJEA LONDON JULAI.

MWANARIADHA nyota wa mbio fupi kutoka Jamaica, Usain Bolt anaweza kuwepo katika michuano ya kudhimisha mwaka mmoja wa michuano ya olimpiki iliyofanyika London mwaja baada ya wakala wake kubainisha kuwa wamefanya mazungumzo yenye kutia matumaini. Mbali na michuano ya olimpiki, Bolt hajashiriki mbio zozote zilizofanyika nchini Uingereza toka mwaka 2009 kwasababu ya sheria zao za kodi ambayo ilikuwa ikimlazimu kuacha kiasi cha pesa katika mbio zozote atazoshiriki na kukatwa makato katika pesa zozote anazopata kutokana na mikataba mingine. Hatahivyo msamaha kwa ajili ya wanariadha wasio wazawa uliondolewa katika bajeti hivyo kuwepo kwa uwezekano mkubwa kwa Bolt kushiriki michuano hiyo ambayo inatarajiw akufanyika Julai 26 hadi 28 mwaka huu. Waandaaji wa michuano hiyo wanamatumaini Bolt atarejea tena Uingereza katika michuano hiyo ikiwa kama sehemu ya maandalizi yake kwa ajili ya michuano ya radha ya Dunia inayotarajiwa kufanyika jijini Moscow baadae mwaka huu. Bolt mwenye umri wa miaka 26 alinyakuwa medali tatu za dhahabu katika michuano ya olimpiki mwaka jana, akiweka rekodi ya olimpiki katika mbio za mita 100 na kusaidia wanariadha wenzake kuweka rekodi mpya ya dunia katika mbio za kupokezana vijiti za mita 400.

Friday, March 29, 2013

TEKNOLOJIA YA KOMPYUTA KATIKA MSTARI WA GOLI GHALI SANA - PLATINI.

RAIS wa Shirikisho la Soka barani Ulaya-UEFA, Michel Platini amesema mfumo wa teknologia ya kompyuta kwenye mstari wa goli ni ghali sana kuutumia katika michuano ya Ligi ya Mabingwa. Platini amesema ni bora fedha hizo akazitumia katika kuinua soka la vijana na miundombinu kuliko kuzitumia kwa ajili ya kufunga mfumo huo. Platini aliongeza kuwa anafurahia uamuzi wa kutumia mfumo wa waamuzi watano katika Ligi ya Mabingwa na Europa League. Amesema gharama za kufunga mfumo huo katika viwanja 280 vinavyotumika kwa ajili ya michuano hiyo inafikia kiasi cha paundi milioni 46 katika kipindi cha miaka mitano hivyo anaona ni gharama kubwa sana kwa makosa ambayo yanaweza kufanyika mara moja katika kipindi cha miaka 40. Shirikisho la Soka Duniani-FIFA limepanga kutumia mfumo huo katika michuano ya Kombe la Dunia mwaka 2014 nchini Brazil. 

UEFA KUTANGAZA ZABUNI KWA MIJI ITAKAYOTAKA KUANDAA EURO 2020, APRIL 16.

SHIRIKISHO la Soka barani Ulaya-UEFA limefikia makubaliano ya kufanya zabuni ya mahitaji na sheria zitakazotumika katika michuano ya Ulaya 2020 abayo kwa mara ya kwanza itafanyika katika miji 13 tofauti itakayochaguliwa Septemba mwaka 2014. Katibu Mkuu wa UEFA Gianni Infantino aliviambia vyombo vya habari mara baada ya mkutano ulifanyika jijini Sofia kuwa wamefikia uamuzi wa kutangaza zabuni kwa mahitaji na sheria zitakazotumika kuanzia Aprili 16 mwaka huu. Waombaji watatakiwa kuwasilisha maombi yao ifikapo Aprili 25 ambapo UEFA itapitia zabuni zote katika kipindi cha Mei na Agosti na kuchagua miji 13 ifikapo Septemba mwakani. Mji 12 ambazo zitashinda zabuni hiyo zitapata nafasi ya kuandaa mechi tatu za hatua ya makundi pamoja na mechi moja ya hatua ya timu 16 bora au robo fainali wakati mji uliobakia wenyewe utapata nafasi ya kuandaa mechi mbili za nusu fainali pamoja na fainali.

PISTORIUS KUSHIRIKI MICHUANO YA DUNIA JIJINI MOSCOW.

WAKALA wa mwanariadha mlemavu, Oscar Pistorius amesema mteja wake huyo anaweza kushiriki michuano ya riadha ya Dunia itakayofanyika jijini Moscow baada ya mwaka huu. Pistorius mwenye umri wa miaka 26 ambaye alikimbia katika michuano ya Olimpiki na Paralimpiki jijini London mwaka jana ameshitakiwa kwa kosa la kumuua rafiki wake wa kike lakini ataruhusiwa kusafiri baada ya mawakili wake kupinga baadhi masharti ya dhamana aliyopewa. Wakala huyo Peet van Zyl amesema kama atakuwa yuko tayari na kufuzu, basi hakuna shaka atshiriki michuano hiyo ya dunia itakayofanyika Agosti. Pistorius ambaye anatumia miguu ya bandia katika kukimbia anatuhumiwa kumuua rafiki yake wa kike Reeva Steenkamp ambaye alipigwa risasi na kufa nyumbai kwake Februari 14 mwaka huu.

FERDINAND ASHANGAZWA NA MASHABIKI WA UINGEREZA.

BEKI wa klabu ya Manchester United, Rio Ferdinand ameonyesha kushangazwa na tukio la kibaguzi la mashabiki wa soka wa Uingereza lililomlenga yeye pamoja na ndugu yake Anton wakati wa mechi dhidi ya San Marino ambayo nchi hiyo ilishinda kwa mabao 8-0. Mashabiki hao ambao walikuwa wakipiga kelele za nyani kuwalenga Rio ambaye alijitoa katika kikosi cha Uingereza kutokana na maumivu ya mgongo na ndugu yake Anton ambaye anacheza katika klabu ya Queens Park Rangers-QPR. Ferdinand aliandika katika ukurasa wa mtandao wa kijamii wa twitter akielezea kusikitishwa kwake na kitendo hicho haswa kutoka kwa mashabiki wan chi yake mwenyewe. Rio amekuwa katika maelewano yasiyo mazuri na baadhi ya wachezaji wa Uingereza toka ndugu yake Anton afanyiwe vitendo vya kibaguzi na nahodha wa zamani wa Uingereza John Terry.

SHARAPOVA, WILLIAMS KUKWAANA FAINALI SONY OPEN.

MWANADADA nyota katika tenisi Maria Sharapova amefanikiwa kutinga fainali ya michuano ya wazi ya Sony ambapo sasa atachuana na Serena Williams. Williams ambaye anashika namba moja katika orodha za ubora duniani alihitaji dakika 65 kumfunga bingwa mtetezi wa michuano hiyo Agnieska Radwanska kwa 6-0 6-3 wakai Sharapova alimgaragaza Jelena Jankovic kwa 6-2 6-1. Pamoja na kiwango kizuri alichonacho Sharapova ambaye ni raia wa Urusi, Williams ndio anapewa nafasi kubwa ya kunyakuwa taji hilo ambapo katika mechi 12 walizokutana Williams ameshinda 10. Kwa upande wa wanaume bingwa wa michuano ya US Open na olimpiki Andy Murray amefanikiwa kutinga hatua ya nusu fainali ya michuano hiyo baada ya kumfunga Marin Cilic wa Croatia kwa 6-4 6-3. Murray raia wa Uingereza ambaye anashika namba mbili katika orodha za ubora duniani kwa upande wa wanaume anatarajiwa kuchuana na Richard Gasquet wa Ufaransa katika kutafuta nafasi ya kucheza fainali ya michuano hiyo Jumapili. 

Thursday, March 28, 2013

MIAMI HEAT YASHINDWA KUENDELEZA UBABE MBELE YA CHICAGO BULLS.

TIMU ya mpira wa kikapu ya Miami Heat imeshindwa kuweka rekodi ya kufikisha michezo 33 bila kupoteza baada ya kufungwa na Chicago Bulls katika mchezo wa Ligi Kuu ya mpira huo nchini Marekani maarufu kama NBA. Heat ambao wamecheza mechi 27 bila kupoteza, wameshindwa kufikia rekodi ya mechi 33 iliyowekwa na timu ya Los Angeles Lakers katika msimu wa mwaka 1971-1972. Nyota Heat LeBron James ambaye ndio mchezaji mwenye thamani zaidi wa NBA amesema hakuna aibu yoyote kwao kushindwa kufikia rekodi hiyo. Katika mchezo huo James ambaye alikuwapo katika kikosi cha Marekani kilichonyakuwa medali ya dhahabu katika michuano ya Olimpiki 2012 alifunga alama 32 lakini juhudi hizo hazikuweza kuinusuru timu yake kupokea kipigo cha vukapu 101-97 kutoka kwa Chicago.

BONANZA LA WAANDISHI WA HABARI LAHAMISHIWA TCC CHANG'OMBE.

BONANZA la vyombo mbalimbali vya habari lililopangwa kufanyika Aprili 6 mwaka huu viwanja vya Leaders Klabu likiandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA), sasa litafanyika viwanja vya Sigara (TCC), Chang’ombe pia Dar es Salaam. Uamuzi wa kuhamisha bonanza hilo umechukuliwa na sekretarieti ya TASWA kutokana na maombi ya waandishi wengi wa michezo kwa vile siku hiyo kuna mechi ya Kombe la Shirikisho la Soka Afrika kati ya timu yasoka ya Azam na Barrack Young Controllers ya Liberia itakayofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam siku hiyo. Azam ni timu pekee ya Tanzania iliyobaki kwenye michuano ya Afrika kwa ngazi ya klabu baada ya Simba na Jamhuri ya Pemba kutolewa katika raundi ya awali. Tunaamini kwa bonanza kufanyika Sigara itakuwa rahisi kwa wadau wetu kushiriki kwenye bonanza na wale wengine watakaohitaji kwenda uwanjani wafanye hivyo wakitokea Sigara kwa hakuna umbali mrefu na kisha warejee kujumuika na wenzao mpaka mwisho. Tunawaomba radhi kwa mabadiliko hayo, lakini yakiwa na lengo la kujenga na kuwa pamoja na wenzetu wa Azam kuhakikisha tunashirikiana nao kwa namna mbalimbali siku hiyo. Bonanza hili linadhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) likiwa na lengo la kuwaweka pamoja waandishi wote wa habari bila kujali ni wa siasa, michezo, uchumi, afya na mambo mengine pamoja na wafanyakazi wa vyombo mbalimbali vya habari ili kubadilishana mawazo na kufurahi pamoja. Bonanza hilo ambalo litahusisha wadau 1,500 kutoka vyombo mbalimbali vya habari litaambatana na michezo mbalimbali itakayohusisha vyombo vyote vitakavyoshiriki na pia kutakuwa na burudani ya muziki kutoka katika moja ya bendi kubwa za muziki wa dansi hapa nchini, ambayo itatangazwa siku zijazo.

FIFA KUCHUNGUZA TUKIO LA SUAREZ.

SHIRIKISHO la Soka Duniani-FIFA linaangalia tukio la ugomvi lililomhusisha mshambuliaji nyota wa Liverpool Luis Suarez katika mchezo baina ya timu yake ya taifa ya Uruguay na Chile Jumanne iliyopita. Tukio hilo lilitokea wakati mchezaji wa Chile Gonzalo Jara alipokuwa amekabana na Suarez na baadhi picha zinamuonyesha mchezaji huyo akimpiga ngumi kwa makusudi Jara ambaye anacheza katika klabu ya Nottingham Forest. Wawili hao walionekana kujibizana maneno baada ya tukio hilo lakini mwamuzi Nestor Pitana aliyechezesha pambano hilo hakuchukua hatua yoyote. Katika taarifa yake FIFA wamedai kuwa bado wanakusanya taarifa za mchezo huo huku wakisubiri nyingine kutoka kwa waamuzi ambazo zitawasilishwa katika muda wa saa 24. Suarez na Jara ambaye ancheza kwa mkopo Forest akitokea klabu ya West Bromwich walikuwa wakigombea nafasi katika eneo la hatari katika mchezo huo huo wa kufuzu michuano ya Kombe la Dunia ambao Chile ilishinda kwa mabao 2-0.

FIFA KUICHUKULIA HATUA MONTENEGRO.

SHIRIKISHO la Soka Duniani-FIFA linakusanya vielelezo ambavyo vinaweza kupelekea kuichukulia hatua Montenegro baada ya taarifa ya kuwepo kwa vurugu kutoka kwa baadhi ya mashabiki wake kwa wachezaji wa Uingereza katika mchezo baina ya nchi hizo ambao walitoka sare ya bao 1-1. Taarifa kutoka gazeti moja nchini Uingereza ilidai kuwa beki wa Uingereza Ashley Cole alitemewa mate wakati golikipa Joe Hart alikuwa akitupiwa vitu wakati wa mchezo huo uliochezwa jijini Podgorica. Uchunguzi wa FIFA katika tukio hilo utaanzia kwenye ripoto ya mwamuzi Jonas Eriksson aliyechezesha mtanange huo. Akihojiwa kuhusu tukio hilo Hart amekiri kurushiwa vitu mbalimbali ikiwemo tishu lakini amesema katika mechi kama hizo matukio kama hayo yamekuwa ya kawaida kwa mashabiki wa timu pinzani ili kujaribu kukuvunja moyo.

CAF YAIFUNGULIA LIBYA.

SHIRIKISHO la Soka barani Afrika-CAF limeondoa adhabu ya kuifungia Libya kuandaa michuano ya soka. CAF iliifungia nchi hiyo iliyopo kaskazini mwa bara la Afrika kuandaa michuano ya Afcon kufuatia vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyoikumba nchi hiyo mwaka 2011. Timu ya taifa pamoja na klabu mbalimbali nchini humo zimekuwa zikicheza mechi zake za nyumbani katika nchi nyingine hususani Morocco, hata hivyo katika uamuzi mpya uliotolewa utaruhusu klabu ya Al-Nasr Benghazi kucheza mechi ya Kombe la Shirikisho AS Far ya Morocco katika uwanja wa nyumbani mwezi ujao. Nchi ya Libya ilibadilishana miaka kwa kuiachia Afrika Kusini kuandaa michuano ya Mataifa ya Afrika-Afcon mwaka 2013 na wao wataandaa michuano ya 2017. Waziri wa Michezo wan chi hiyo Abdessalem Ghouila amesema kuandaa michuano ya Afcon 2017 kutasaidia kuiridusha nchi hiyo katika hali ya kawaida baada ya vurugu za mapigano ambazo zilipelekea watu zaidi ya 25,000 kupoteza maisha.

UWANJA WA OLIMPIKI BRAZIL WAFUNGWA.

UWANJA ambao umepangwa kutumika kwa ajili ya michuano ya Olimpiki 2016 itakayofanyika nchini Brazil umefungwa kwa muda usiojulikana kwasababu ya matatizo ya kimiundo mbinu katika paa lake. Uwanja huo uitwao Joao Havelange lilikiwa ni jina la rais wa zamani wa Shirikisho la Soka Duniani-FIFA uliopo jijini Rio de Janeiro ulijengwa miaka sita iliyopita. Ndio uwanja uliokuwa ukitumika katika mechi mbalimbali za soka jijini humo wakati Uwanja wa Maricana ukiwa umefungwa kwa matengenezo kwa ajili ya michuano ya Kombe la Dunia mwakani. Mamlaka zinazohusika pia zilikiri kuchelewa kwa ukarabati wa Maricana na tatizo la fedha katika matengenezo ya viwnaja vingine ambavyo vitatumika kwa ajili ya mechi za ufunguzi za Kombe la Dunia. Meya wa jiji hilo Eduardo Paes alithibisha kuufunga uwanja huo kwa matengenezo baada ya kupokea taarifa za kiufundi kuwa paa lake haliko salama kwa matumizi.

PEDRO NJE WIKI MBILI.

MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Hispania na klabu ya Barcelona, Pedro anaweza kukosa mechi mbili za klabu yake baada ya kuumia msuli wakati akiitumikia timu yake ya taifa katika mchezo wa kundi I dhidi ya Ufaransa. Nyota huyo alitolewa nje katika dakika ya 76 Jumanne iliyopita baada ya kuifungia bao la mapema timu yake dhidi ya Ufaransa ambayo inanolewa na Didier Deschamps na kuipaisha timu hiyo kileleni wa msimamo wa kundi lao. Maumivu hayo ya msuli yanaweza kumfanya mchezaji huyo kukosa mechi ya Ligi Kuu nchini Hispania maarufu kama La Liga kati ya timu yake Barcelona dhidi ya Celta Vigo Jumamosi na mchezo mwingine dhidi ya Real Mallorca mwishoni mwa wiki ijayo. Pamoja na maumivu hayo tayari ilishathibitishwa kuwa Pedro atakosa mchezo wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa Ulaya hatua ya robo fainali dhidi ya Paris Saint-Germain wiki ijayo baada ya kupata kadi ya pili ya njano katika mchezo dhidi ya AC Milan.

Wednesday, March 27, 2013

VAN PERSIE AMUACHA CRUYFF SASA AMUWINDA KLUIVERT.

MSHAMBULIAJI nyota wa kimataifa wa Uholanzi na klabu ya Manchester United Robin van Persie amefanikiwa kuipita rekodi ya mabao ya nguli wa soka wa nchi hiyo Johan Cruyff baada ya kufunga mabao mawili katika ushindi wa mabao 4-0 iliyopata timu yake. Cruyff ambaye anahesabiwa kama mmoja wa wachezaji bora katika historia ya soka nchini humo, alifunga mabao 33 katika mechi 48 za kimataifa alizocheza na rekodi hiyo sasa imepitwa na Van Persie ambaye amefikisha mabao 34. Mshambuliaji huyo sasa amebakisha mabao sita ili kumfikia mshambuliaji nyota wa zamani Patrick Kluivert ambaye aliweka rekodi ya kuwa mfungaji bora wa kipindi chote wa nchi hiyo kwa kufunga mabao 40. Uholanzi sasa inahitaji alama sita zaidi katika mechi zao nne zilizobakia katika kundi D ili kujihakikishia nafasi ya kushiriki michuano ya Kombe la Dunia mwaka 2014 itakayofanyika nchini Brazil.

HAYE KUMTAJA MPINZANI WAKE KESHO.

BINGWA wa zamani wa ngumi wa uzito wa juu, David Haye anatarajia kutangaza pambano lake la kwanza toka alipopigana mara ya mwisho Julai mwaka jana. Haye mwenye umri wa miaka 32 alimtandika Dereck Chisora mwaka uliopita katika pambano ambalo liliwekewa vikwazo na Mamlaka ya Ngumi nchini Luxembourg. Bodi ya Ngumi nchini Uingereza iliwanyang’anya leseni mabondia hayo kufuatia kufanya vurugu na kutaka kuzipiga kavu kavu jijini Munich, Ujerumani Februari mwaka uliopita. Mara kwa mara Haye amekuwa akionyesha nia ya kupigana na bingwa wa dunia wa WBC Vitali Klitschko ingawa hata hivyo bondia huyo amekuwa akimkwepa. Kaka yake Vitali, Wladimir bingwa wa mikanda ya IBF, WBO na WBA ambaye alimtandika Haye mwaka 2011 anatarajiwa kukutana na Francesco Pianeta Mei mwaka huu.

Tuesday, March 26, 2013

TAARIFA MBALIMBALI KUTOKA TFF LEO.

TENGA AHIMIZA VIGEZO U15 FIFA COPA COCA-COLA
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga amewataka viongozi wa vyama vya mpira wa miguu vya mikoa kuhakikisha wanaingiza wachezaji wenye umri sahihi katika michuano ya U15 FIFA Copa Coca-Cola 2013. Ametoa mwito huo leo (Machi 26 mwaka huu) wakati akifungua semina elekezi ya michuano ya Copa Coca-Cola ambayo kuanzia mwaka huu itakuwa ikishirikisha watoto wenye umri chini ya miaka 15. Rais Tenga amesema hakuna jambo la kipuuzi kama kuchomekea wachezaji ambao wamezidi umri unaotakiwa kwa vile lengo la michuano ya aina hiyo ni kubaini vipaji na kuwafanya watoto wapende kucheza mpira wa miguu. “Kwanza nawashukuru kwa kutenga muda wenu na kuhudhuria semina. Lakini ni vizuri pia mkahakikisha mnakuwepo kwenye mashindano ili kutekeleza haya ambayo tutakubaliana katika semina hii. Mkileta mtu mwingine anaweza kutuanzishia mambo mengine badala ya yale tutakayokubaliana,” amesema Tenga. Pia ameishukuru kampuni ya Coca-Cola ambaye imekuwa ikidhamini michuano hiyo tangu mwaka 2007 ambapo semina hiyo elekezi inayoshirikisha makatibu wa vyama vya mpira wa miguu vya mikoa na waratibu wa mikoa wa michezo ya UMISSETA ni ya saba mfululizo. Ratiba ya michuano hiyo kuanzia mwaka huu imebadilika ambapo sasa itaanzia ngazi ya wilaya Aprili wakati fainali katika ngazi ya Taifa itachezwa Septemba.

SIMBA, KAGERA SUGAR KUPAMBANA VPL
Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania inaendelea kesho (Machi 27 mwaka huu) kwa mechi mbili ambapo bingwa mtetezi Simba atakuwa mgeni ya Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba. Uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 3,000 unatarajiwa kushuhudia mechi yenyen ushindi kutokana na uwezo wa wachezaji wa pande zote mbili. Mechi nyingine itapigwa kwenye Uwanja wa Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam kati ya wenyeji Azam na Tanzania Prisons kutoka Mbeya.

VILANOVA ATUA BARCELONA.

KLABU ya Barcelona ya Hispania, imetangaza kuwa kocha wa klabu hiyo ambaye alikuwa jijini New York kwa matibabu ya kansa toka Januari mwaka huu amerejea nchini humo leo. Katika taarifa iliyotumwa katika mtandao wa klabu hiyo imethibitisha kuwa kocha huyo tayari yuko jijini Barcelona tayari kuendelea kuendelea na majukumu yake katika klabu hiyo baada ya kuwa nje kwa kipindi cha miezi miwili. Vilanova mwenye umri wa miaka 44 aliondoka kwenda New York kwa matibabu zaidi ya mionzi Januari na katika kipindi hichochote msaidizi wake Jordi Roura ndio alikuwa akiisimamia timu hiyo. Taarifa hiyo pia ilidai kuwa Roura na Aureli Altimira ambao ndio waliompokea Vilanova wakati aliporejea ndio wataongoza mazoezi ya timu hiyo leo mchana huku Vilanova mwenyewe akitarajiwa kuchukua nafasi yake hatua kwa hatua.

10,000 KURUHUSIWA KUISHANGILIA MISRI.

MASHABIKI wapatao 10,000 wanatarajiwa kuruhusiwa kuishangilia timu yao ya taifa ya Misri wakati wa mchezo wa kutafuta tiketi ya kucheza michuano ya Kombe la Dunia dhidi ya Zimbabwe ikiwa ni hatua moja kubwa ya kuirejesha nchi hiyo katika hali ya kawaida kimichezo. Misri pia wanafikiri uwepo wa mashabiki uwanjani katika mchezo huo utaongeza nafasi yao ya kufuzu michuano hiyo itakayofanyika nchini Brazil mwkaani kwa mara ya kwanza baada ya miaka zaidi ya 20 kupita. Wizara ya Mambo ya Ndani ya nchi hiyo inatarajia kuruhusu idadi hiyo ya mashabiki katika Uwanja wa Borg El Arab uliopo katika pwani ya Mediterranean toka walipozuia kufanya hivyo baada ya vurugu za kisiasa zilizopelekea mashabiki wapatao 70 kupoteza maisha katika mchezo wa ligi huko Port Said mwaka mmoja uliopita. Vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Misri toka kuangushwa kwa utawala wa aliyekuwa rais wan chi hiyo kwa kipindi kirefu Hosni Mubarak pia viliathiri soka na kupeleka kushindwa kufuzu kushiriki michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa kipindi cha miaka miwili.

BRAZIL BADO IKO VIZURI - SCOLARI.

KOCHA wa timu ya taifa ya Brazil, Luiz Felipe Scolari amesisitiza kuwa kikosi chake kiko katika njia sahihi baada ya kutoa sare dhidi ya Urusi Jumatatu usiku. Brazil ilihitaji bao la dakika za mwisho lilifungwa na mshambuliaji wa klabu ya Fluminense Fred ili kupata sare hiyo kutoka kwa Urusi inayonolewa na kocha Fabio Capello katika mchezo huo wa kimataifa wa kirafiki uliofanyika katika Uwanja wa Stamford Brigde. Scolari ameshindwa kuipa ushindi Brazil toka achukue mikoba tena ya kuinoa ambapo mbali na sare hiyo lakini pia alitoa sare ya mabao 2-2 na Italia wiki iliyopita huku akikubali kipigo cha mabao 2-1 kutoka kwa Uingereza Februari mwaka huu. Akihojiwa mara ya mchezo huo Scolari amesema kuwa katika mechi dhidi ya Italia na Urusi wamecheza kwa kiwango kizuri lakini aliwataka watu wasisahau kuwa walikuwa wakicheza na timu ambazo zilikuwa zimejipanga vizuri. Brazil inakabiliwa na mchezo mwingine wa kimataifa wa kirafiki dhidi ya Chile April 24.

KOCHA WA DRC ALALAMIKIA UMRI MKUBWA WA WACHEZAJI KATIKA MICHUANO YA VIJANA YA AFRIKA.

KOCHA wa timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 20 ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo-DRC Sebastian Migan amebainisha kuwa timu yake ingesonga mbele katika hatua ya nusu fainali ya michuano ya Vijana ya Afrika kama timu zingine zingefuata sheria. DRC ilishindwa kufuzu hatua hiyo baada ya kukubali kipigo cha mabao 3-1 dhidi ya Nigeria katika mchezo uliochezwa Jumamosi iliyopita katika Uwanja wa Ahmed Zabana. Migan amedai kuwa baadhi ya timu katika michuano hiyo wamekuwa wakidanganya umri wa wachezaji wao na kutaka maofisa wanaosimamia michuano hiyo kulifuatilia kwa makini suala hilo. Kocha amesema iko wazi kwangu na kwa wengine kuwa wachezaji wengi katika timu ya Nigeria walikuwa wamezidi umri zaidi ya miaka 20 lakini amefurahishwa na jinsi wachezaji wake walivyojituma pamoja na kwamba wametolewa. Nigeria ambao wanatuhumiwa kutumia vijeba katika michuano hiyo wanatarajiwa kuchuana na Misri katika Uwanja wa Oumr Ouciaf baadae leo.

SHARAPOVA, SERENA HAWASHIKIKI MICHUANO YA SONY OPEN.

MCHEZA tenisi nyota kutoka Urusi, Maria Sharapova amefanikiwa kusonga mbele katika michuano ya wazi ya Sony kwa kumfunga Klara Zakopalova wa Jamhuri ya Czech. Sharapova alimfunga Zakopalova kwa 6-2 6-2 na kujikatia tiketi ya kucheza robo fainali ya michuano hiyo inayofanyika huko Miami, Florida nchini Marekani. Mapema mwanadada anayeshika namba moja katika orodha za ubora wa mchezo huo Serena Williams naye alifanikiwa kusonga mbele baada ya kumfunga Dominika Cibulkova wa Slovakia. Katika mchezo huo Williams ilibdi atumie uzoefu wake baada ya kupoteza seti ya kwanza lakini alifanikiwa kuzinduka na kumfunga Cibulkova kwa 2-6 6-4 6-2.

WOODS KINARA WA GOFU DUNIANI KWA MARA NYINGINE.

MCHEZAJI gofu nyota Tiger Woods amerejea katika nafasi ya kwanza katika orodha za wachezaji bora wa mchezo huo duniani toka mwaka Octoba mwaka 2010 baada ya kushinda michuano ya Arnold Palmer Invitational. Woods mwenye umri wa miaka 37 alichukua nafasi hiyo iliyokuwa ikishikiliwa na Rory McIlrol aliyekuwa akishika nafasi hiyo toka Novemba mwaka 2011. Hilo linakuwa ni taji la 77 la mashindano ya PGA kwa Woods ambaye ni raia wa Marekani na tatu kwa mwaka huu 2013. Akihojiwa mara baada ya kushinda mchezo huo Woods amesema ilikuwa michuano mizuri na anafurahi kurejea katika nafsi ya kwanza baada ya kusota kurejea katika kiwango chake kwa kipindi kirefu. Amesema ushindi huo wa taji la PGA unamuweka vyema kabla ya kuanza kwa msimu mpya akijaribu kufukuzia taji la tano la michuano mikubwa ya Masters ambayo inatarajiwa kuanza April 11 mwaka huu.

ENYEAMA ASHINDWA KUTIMIZA AHADI.

GOLIKIPA wa Nigeria, Vincent Enyeama amethibitisha kuwa alivunja ahadi yake ya kucheza huku akiwa amevua bukta yake kufuatia timu ya taifa ya nchi hiyo kunyakuwa michuano ya Mataifa ya Afrika-Afcon iliyofanyika nchini Afrika Kusini. Katika mahojiano yake na mtandao wa supersport jijini Faro, Ureno mapema Januari, Enyeama alidai kuwa kama Nigerian ikitawazwa mabingwa wa Afrika ndoto zake zitakuwa zimetimia na kwa furaha atacheza huku akiwa amevua bukta yake. Lakini golikipa alipohojiwa kuhusu ahadi yake hiyo aliyotoa alidai kuwa hakuitmiza kwasababu haikumlazimu kufanya hivyo kwani sio ahadi zote zinezotolewa na serikali huwa zinatimizwa na hilo linakwenda sambamba na ahadi mbalimbali zinatolewa na watu. Enyeama ambaye ameichezea Nigeria mechi 78 za kimataifa amesema ana sababu zake binafsi za kushindwa kutimiaza ahadi yake aliyotoa mwenyewe.

SUPER EAGLE ITAFUZU KOMBE LA DUNIA - LAMOUCHI.

KOCHA wa timu ya taifa ya Ivory Coast, Sabri Lamouchi anaamini kuwa timu ya taifa ya Nigeria-Super Eagles wanaweza kushinda kikwazo cha kutoa sare ya bao 1-1 dhidi ya Kenya nyumbani na kufuzu michuano ya Kombe la Dunia 2014 itakayofanyika nchini Brazil. Nigeria mbao ni mabingwa wa Afrika walishindwa kutamba Jumamosi baada ya kupata sare katika dakika za lala salama kwa bao lililofungwa na mchezaji aliyetokea benchi Nnamdi Oduamadi lakini Lamouchi amedai kuwa atashangaa kama timu hiyo ikishindwa kwenda nchini Brazil. Kocha huyo amedai kuwa katika safari ya kuelekea nchini Brazil timu yake Ivory Coast lazima iwepo, timu nyingine moja au mbili kutoka Afrika ya Kaskazini, Nigeria na pengine Zambia anadhani ndio timu tano zitakazowakilisha bara la Afrika katika michuano hiyo. Nigeria iliitoa Ivory Coast katika hatua ya robo fainali ya michuano ya Afcon iliyofanyika nchini Afrika Kusini na lamouchi anakiri kuwa hakutegemea kama timu hiyo ingetinga hatua ya nusu fainali mbele ya kikosi chake kilichosheheni nyota lukuki.

Monday, March 25, 2013

COSTA RICA WAKATA RUFANI.

SHIRIKISHO la Soka nchini Costa Rica limekata rufani rasmi kuutaka mchezo wao dhidi ya Marekani ambao walifungwa kwa bao 1-0 urudiwe kutokana na hali mbaya ya hewa iliyoathiri mchezo huo. Bao lililofungwa na Clint Dempsey katika dakika ya 16 ndio bao pekee katika mchezo huo ambao mara kwa mara ulikuwa ukisimamishwa ili kupisha wafanyakazi kutoa barafu nyingi ambazo zilikuwa zikianguka uwanjani. Katika taarifa yao rais wa shirikisho hilo Ronaldo Villalobos amedai kuwa picha za mnato na video vimetumwa Shirikisho la Soka Duniani-FIFA ili kuipa nguvu rufani yao na kuwataka waamuzi waliochezesha mchezo huo kuchukuliwa hatua za kisheria. Pia katika taarifa hiyo Villalobos amedai kuwa katika sheria za soka wafanyakazi hawaruhusiwi kuingia uwanjani wakati wa mchezo ili kusafisha wakati akidai pia ilikuwa kazi kubwa mpira kuchezwa kutokana na barafi nyingi iliyokuwepo. Kocha wa Costa Rica Jorge Luis Pinto alitaka mchezo huo usogezwe mbele lakini kocha wa Marekani Jurgen Klinsmann alisisitiza kuwa ni sawa mchezo huo kuendelea kwakuwa wachezaji wa pande zote mbili wanakumbana na hali hiyo. Matokeo hayo ya Ijumaa yanaifanya Costa Rica kushika mkia katika kundi lao wakiwa na alama moja katika mechi mbili walizocheza huku Marekani wakiwa katika nafasi ya pili kwa kupata alama tatu.

MUNTARU AWAPONGEZA MASHABIKI JIJINI KUMASI.

NAHODHA wa kikosi cha timu ya taifa ya Ghana, Sulley Muntari amewapongeza mashabiki wa soka wa nchi hiyo waliojitokeza kuishangilia timu yao wakati wakicheza mchezo wa kufuzu michuano ya Kombe ya Dunia dhidi ya Sudan uliofanyika katika Uwanja wa Baba Yara jijini Kumasi. Katika mchezo huo Ghana ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa mabao 4-0 na kuweka matumaini hai ya kukata tiketi ya kucheza michuano hiyo ambapo Muntari alikuwa akicheza mchezo wake wa kwanza toka aumie mguu. Muntari amesema ushindi huo ulikuwa mzuri kwao kwasababu Zambia ambao wako nao kundi moja wenyewe walitoka bila ya kufungana na Lesotho, na ushindi huo utawasaidia katika mchezo mwingine wa ugenini dhidi ya hao hao Sudan na ni mategemeo yao watashinda tena. Mabao ya Ghana katika mchezo huo yalifungwa na Asamoah Gyan, Mubarak Wakaso, Abdul Majeed Waris na Emmanuel Badu na ushindi huo unaifanya Ghana kuisogelea Zambia ambao wanaongoza kundi lao kwa tofauti ya alama moja huku kukiwa kumebakia michezo mitatu.

FRANKFURT YAMUONGEZA MKATABA VEH.

KLABU ya Eintracht Frankfurt ya Ujerumani imebainisha kuwa kocha Armin Veh amekubali kuongeza mkataba wa kuinoa klabu hyo kwa msimu mwingine mmoja mpaka mwaka 2014. Veh ambaye alijiunga na klabu hiyo mwaka 2011 aliiongoza timu hiyo kurejea katika nafasi za juu kwenye msimamo wa Ligi Kuu nchini humo maarufu kama Bundesliga ambapo sasa timu hiyo inafukuzia nafasi ya kushiriki michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Katika taarifa iliyotolewa na rais wa klabu hiyo Heribert Brunchhagen amesema amefurahi kumshawishi kocha huyo kuendelea kuwepo hapo haswa kutokana na kuingoza vyema klabu hiyo msimu huu. Mbio za Frankfurt msimu huu ni kutafuta nafasi ya nne lakini Veh amepania kukisuka upya kikosi chake msimu ujao kwa ajili kutafuta nafasi za juu zaidi au kunyakuwa taji la Bundesliga.

VILANOVA KUREJEA NYUMBANI BAADA YA MIEZI MIWILI YA MATIBABU.

KLABU ya Barcelona imebainisha kuwa kocha wake Tito Vilanova atarejea nyumbani wiki hii baada ya kukaa jijini New York Marekani alipokuwa akipatiwa matibabu ya mionzi ya kansa. Vilanova mwenye umri wa miaka 44 alifanyiwa upasuaji wa koo kuondoa uvimbe wa kansa Desemba 20 mwaka jana na baadae kuanza tiba ya mionzi kwa muda wa wiki sita. Kocha aliondoka kuelekea New York kwa matibabu zaidi Januari na sasa yuko tayari kurejea nyumbani tena baada ya kukaa huko marekani kwa miezi miwili. Vilanova alichukua nafasi ya Pep Guardiola katika kipindi cha majira ya kiangazi mwaka jana na kupewa mkataba wa mwaka mmoja ambapo wakati akiwa katika matibabu nafasi yake ilikuwa ikishikiliwa na kocha msaidizi Jordi Roura.

TAARIFA MBALIMBALI KUTOKA TFF LEO.

MECHI YA TAIFA STARS YAINGIZA MIL 226/-
Mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia kati ya Tanzania (Taifa Stars) na
Morocco (Lions of the Atlas) iliyochezwa jana (Machi 24 mwaka huu) na
Stars kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 imeingiza sh. 226,546,000. Fedha hizo zimepatikana kutokana na watazamaji 32,614 waliokata tiketi
kushuhudia mechi hiyo kwa kiingilio cha sh. 5,000, sh. 7,000, sh.
10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000. Mgawanyo wa mapato hayo ulikuwa kama ifuatavyo; asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ni sh. 34,557,864.41, maandalizi ya mchezo sh. 28,450,000 wakati wa gharama za uchapaji tiketi ni sh. 8,625,641.88. Nyingine ni bonasi kwa timu ya Taifa Stars sh. 28,798,220.34, asilimia 15 ya uwanja sh. 18,917,141.01, asilimia 20 ya gharama za mechi sh.25,222,854.67 na asilimia 5 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika(CAF) sh. 6,305,713.67. Asilimia 60 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) sh. 71,885,135.82 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 3,783,428.20 ambayo ni asilimia 5 kutoka kwenye mgawo wa TFF.


TENGA AWAPONGEZA WACHEZAJI, SERIKALI
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga
ameipongeza wachezaji wa Taifa Stars na benchi lao la ufundi,
washabiki, mdhamini na Serikali kwa kufanikisha ushindi wa jana. Tenga amesema ushindi huo umetokana na ushirikiano kutoka kwa wadau wote, na hasa wachezaji walioonesha kiwango kikubwa kulinganisha na mechi zilizopita ikiwemo kiwango cha kujituma uwanjani. Amesema Serikali ni mdau mkubwa wa mpira wa miguu katika miundombinu, usalama na idara zake mbalimbali ikiwemo Uhamiaji ambayo imefanikisha kwa kiasi kikubwa kuwepo kwa mechi hiyo ambapo Taifa Stars iliifunga Morocco mabao 3-1.


MKUTANO WA DHARURA SIMBA SI HALALI
Mkutano Mkuu wa Dharura ulioitishwa na wanachama wa Simba, Machi 17 mwaka huu na kuuondoa uongozi wa klabu hiyo si halali kwa vile haukufuata taratibu, na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) halitambui Kamati za Muda. Uamuzi huo umefikiwa na Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za
Wachezaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana jana (Machi 24 mwaka huu) jijini Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wake Alex Mgongolwa. Kamati imebaini kuwa kwa mujibu wa Ibara ya 22(2) ya Katiba ya Simba, Mkutano Mkuu wa Dharura unaitishwa na Kamati ya Utendaji baada ya
wanachama wasiopungua 500 kuwasilisha ombi hilo kwa maandishi na
kujiorodhesha. Mkutano huo haukuitishwa na Kamati ya Utendaji ya
Simba. Utaratibu huo haukufuatwa ambapo barua ya Mkutano huo iliandikwa kwa Msajili wa Klabu na Vyama vya Michezo badala ya Kamati ya Utendaji ya
Simba ambayo ndiyo matakwa ya Katiba ya Simba. Kwa mujibu wa Katiba ya Simba, Kamati ya Utendaji ndiyo inayoitisha Mkutano Mkuu wa Dharura baada ya kuhakiki uhai na uhalali wa wanachama waliojiorodhesha kuomba mkutano huo. Kamati imesisitiza kuwa Katiba za wanachama wote wa TFF hazina
kipengele cha kura ya kutokuwa na imani na uongozi (vote of no confidence), ndiyo maana uko nyuma wanachama wa Yanga, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Shinyanga (SHIREFA) na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Tabora (TAREFA) walipiga kura hiyo, na TFF kutotambua uamuzi wao. Hata Katiba ya Simba haitoi mamlaka kwa Mkutano Mkuu wa Dharura kufukuza uongozi uliochaguliwa. Katiba za wanachama wote wa TFF zimezingatia katiba mfano za Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) ambazo zinasema
kiongozi ataingia madarakani kwa uchaguzi, na si kuteuliwa (Kamati ya
Muda). Pia Kamati imesema endapo wanachama wa Simba wangefuata taratibu na uongozi ukakataa kuitisha mkutano, wanachama wangetuma ombi hilo TFF kupitia Kamati ya Sheria ili kutoa mwongozo kwa uongozi wa Simba .
TFF ina mamlaka ya kutoa adhabu kwa viongozi wa wanachama wake
wanaokwenda kinyume cha Katiba zao. Pia Kamati imesisitiza kwa
wanachama wa TFF kuitisha mikutano yao kwa mujibu wa taratibu na
Katiba zao, na wale ambao muda umefika wafanye hivyo haraka.


TENGA KUFUNGUA SEMINA ELEKEZI COPA COCA COLA
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga
atakuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa semina elekezi ya michuano ya
Copa Coca Cola itakayofanyika kesho (Machi 26 mwaka huu). Semina hiyo inayoshirikisha makatibu wakuu wa vyama vya mpira wa miguu
mikoa ya Tanzania Bara na Zanzibar itafanyika Uwanja wa Taifa, Dar es
Salaam na itafunguliwa na Rais Tenga kuanzia saa 3 kamili asubuhi. Washiriki wengine katika semina hiyo itakayokuwa na watoa mada kutoka
TFF na wadhamini kampuni ya Coca Cola ni waratibu wa michuano ya Umoja
wa Michezo wa Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA).

WACHEZAJI WA JAMHURI YA AFRIKA YA KATI WASHINDWA KUREJEA NYUMBANI BAADA YA WAASI KUCHUKUA NCHI.

WACHEZAJI wa timu ya taifa ya Jamhuri ya Afrika ya Kati wanatarajiwa kuchelewa kurejea nyumbani baada ya waasi kuuteka mji mkuu wa nchi hiyo wakati wachezaji hao wakiwa Afrika Kusini kucheza mechi ya kufuzu michuano ya Kombe la Dunia. Chama cha Soka nchini Afrika Kusini-SAFA kimesema kuwa timu hiyo inatarajiwa kuondoka nchini humo kwa makundi mawili lakini hakuna kundi hata moja litakaloelekea nyumbani kwasasa. Wachezaji wan chi hiyo wanaocheza soka la kulipwa barani Ulaya watasafiri kuelekea Paris baadae leo, wakati wachezaji wanaosakata kabumbu nyumbani wao watakwenda Douala, Cameroon ambapo watakuwa wakifuatilia hali inavyoendelea nyumbani. Majeshi ya waasi yalifanikiwa kuuteka mji mkuu wan chi hiyo Bangui na kumlazimisha rais aliyekuwepo madarakani kuikimbia nchi yake. Afrika ya Kati ilifungwa mabao 2-0 na Afrika Kusini katika mchezo huo uliochezwa jijini Cape Town Jumamosi.

PELE AFURAHISHWA NA JEMBE LAKE JOSHUA KUANZA KUNG'AA SANTOS.

NGULI wa soka duniani Pele ameonyesha furaha yake baada ya kumshuhudia mwanae wa kiume aitwaye Joshua akicheza katika kikosi cha klabu ya Santos kwenye michuano ya vijana chini ya miaka 17. Ili kuonyesha furaha yake Pele alitumwa picha ya mwanaye huyo mwenye umri wa miaka 16 katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa twitter na kusema kuwa amefurahishwa kumuona mwanae akiwa katika jezi ya Santos. Katika kipindi chake Pele alifunga mabao zaidi 1,000 wakati akicheza Santos na anajulikana kama mmoja wa wachezaji bora kabisa kuwahi kutokea katika kipindi chote. Pele alisajiliwa Santos akiwa na umri wa miaka 15 na kuwa mchezaji mdogo zaidi kuwahi kushinda Kombe la Dunia akiwa na umri wa miaka 17. Wakati akifunga bao lake ya 1000 Novemba 19 mwaka 1969 mashabiki wa Santos walivamia uwanja na kumbeba juu juu na siku imebakia katika kumbukumbu za klabu hiyo ambayo huitwa Pele Day.

VETTEL AMUOMBA RADHI WEBBER.

DEREVA wa mbio za magari ya langalanga, Sebastian Vettel amemuomba radhi dereva mwenzake wa timu ya Red Bull Mark Webber kwa kumpita na kwenda kinyume na maagizo aliyopewa na kupelekea kushinda mbio za Malaysian Grand Prix. Katika mbio hizo Vettel alipewa maagizo na timu yake kupunguza mwendo kwasababu Webber tayari alikuwa akiongoza mbio hizo katika mzunguko wa mwisho lakini dereva huyo alikaidi maagizo hayo kwa kuongeza kasi na kumpita mwenzake na kunyakuwa ubingwa wa mbio hizo. Vettel amesema anajua hakufanya vyema kukaidi amri aliyopewa, haelewi ni kwanini alimua kufanya hivyo ila anaomba radhi kwa timu nzima pamoja na dereva mwenzake. Dereva huyo aliendelea kusema kuwa anajua anahitaji kuwa na maelezo ya kutosha juu ya kilichotokea kwasababu alisikia maelezo aliyopewa vizuri lakini hakuyatekeleza kwasasabu hakuelewa ndio kitu pekee ambacho anaweza kusema kwasasa. Mbio hizo ambazo zilifanyika katika mvua iliyokuwa ikinyesha katika jiji la Kuala Lumpur Vettel alishika namba moja akifuatia wa Webber na nafasi ya tatu ilishikwa na Lewis Hamilton wa timu ya Marcedes.

Saturday, March 23, 2013

HISPANIA YANG'ANG'ANIWA ULAYA.

Mabingwa wa Dunia na Ulaya, Hispania jana walishindwa kutamba baada ya kung’ang’aniwa sare na Finland lakini Uingereza, Ujerumani, Ufaransa na Uholanzi zilifanikiwa kupata ushindi wakati mataifa makubwa yalipokuwa yakitafuta tiketi ya kucheza michuano ya Kombe la Dunia 2014 jana. Hispania ambao waling’ang’aniwa sare ya bao 1-1 na Finland katika mchezo uliochezwa huko jijini Gijon wamepoteza nafasi yao ya kwanza waliyokuwa wakishikilia katika kundi I ambapo sasa Ufaransa ndio wanaongoza kundi hilo baada ya kufanikiwa kuigaragaza Georgia kwa mabao 3-1. Katika michezo mingine Uingereza ilipata ushindi mnono kwa kuichakaza San Marino mabao 8-0 na vigogo wengine Ujerumani wao walipata ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Kazakhstan wakai Uholanzi wao waliibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Estonia mabao ambayo yote yalifungwa katika kipindi cha pili. Ubelgiji wao waliendelea kujisogeza katika kupata nafasi ya kwenda nchini Brazil 2014 baada ya kupata ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Macedonia na kukaa kileleni katika kundi A wakiwa alama sawa na Croatia ambao nao walifanikiwa kuwatandika mahasimu wao Serbia kwa mabao 2-0. Mechi zingine ni Bosnia ilifanikiwa kuifunga Ugiriki kwa mabao 3-1, Ureno walishindwa kutamba mbele ya Israel kwa kung’ang’aniwa sare ya mabao 3-3 na Sweden nao walishindwa kuitambia Ireland kwa kutoka nayo sare ya bila kufungana.

Thursday, March 21, 2013

MWANARIADHA NGULI WA ZAMANI WA MBIO FUPI AFARIKI DUNIA.

MWANARIADHA nyota wa zamani wa mbio fupi kutoka Italia Pietro Mannea ambaye pia alikuwa akishikilia rekodi ya zamani ya mbio za mita 200 amefariki dunia akiwa na miaka 60. Mennea alishinda medali ya dhahabu ya mbio za mita 200 katika michuano ya Olimpiki iliyofanyika jijini Moscow mwaka 1980 akimshinda bingwa wa mbio za mita 100 kutoka Uingereza Alan Wells aliyeshika nafasi ya pili. Mkongwe huyo alivunja rekodi ya dunia ya mbio za mita 200 Septemba mwaka 1979 ambapo alitumia muda wa sekunde 19.72 rekodi ambayo ilidumu kwa kipindi cha miaka 17 mpaka ilipokuja kuvunjwa na Michael Johnson mwaka 1996 ambaye alikimbia kwa kutumia muda wa sekunde 19.66. Rekodi ya Johnson ambaye ni raia wa Marekani ilikuja kuvunjwa na Usain Bolt kutoka Jamaica katika michuano ya olimpiki iliyofanyika jijini Beijing mwaka 2008 akitumia muda wa sekunde 19.19 lakini muda aliotumia Mennea unabakia katika rekodi za Ulaya. Rais wa Kamati ya Olimpiki nchini Italia Giovanni Malago amesema mwili wa Mennea utazikwa katika makao makuu ya kamati hiyo. Hakuna chanzo chochote kilichotajwa kusababisha kifo cha nguli huyo.

NI MMOJA AU WAWILI KUTOKA BARCELONA NA MADRID NDIO WANGEFAA BAYERN - HOENESS.

RAIS wa klabu ya Bayern Munich ya nchini Ujerumani, Uli Hoeness anaamini kuwa wachezaji wawili au watatu kutoka Barcelona na Real Madrid ndio wanaweza kucheza katika kikosi cha kwanza cha vinara hao wa Ligi Kuu nchini humo maarufu kama Bundesliga. Timu hizo mbili kutoka Hispania ndio zinaonekana kuwa na nguvu katika soka duniani kwasasa lakini Hoeness anafikiri Bayern na wenyewe wanaweza kujumuishwa huko kutokana na kikosi imara walichokuwa nacho. Akihojiwa ni wachezaji gani wa Barcelona ambayo angeweza kuwasajili katika kikosi cha Bayern kama angepata nafasi hiyo alimtaja Andres Iniesta na Jordi Alba. Bayern wamekuwa wakihusishwa na kutaka kufanya usajili wa majina makubwa kufuatia kutangaza kuwa Pep Guardiola anatarajiwa kuwa kocha mpya wa klabu hiyo msimu ujao lakini wamekataa kutaja aiana ya wachezaji watakaowahitaji katika kipindi cha majira ya kiangazi.

WOODS NDIO MWANAMICHEZO TAJIRI ZAIDI DUNIANI.

MCHEZAJI nyota wa mchezo wa gofu duniani, Tiger Woods ameendelea kuongoza orodha ya wanamichezo wanaolipwa zaidi duniani kwa kukusanya kiasi cha paundi milioni 39.4 kwa mwaka. Woods ambaye akipambana kurejea katika kiwango chake toka atalikiane na mkewe mwaka 2010 mapato yake mengi yanatokana na mikataba minono aliyonayo katika makampuni mbalimbali ambayo amekuwa akitangaza bidhaa zao. Wengine katika orodha hiyo ni bondia kutoka Philipens, Manny Pacquiao anayekusanya kitita cha paundi milioni 37.7 kwa mwaka akifuatiwa na mchezaji nyota wa mpira wa kikapu katika ligi ya NBA ya Marekani Kobe Bryant anayekusanya paundi milioni 36.8 kwa mwaka. Nyota mwingine wa NBA LeBron James yuko katika nafasi ya nne akikusanya kiasi cha paundi milioni 36 akifuatiwa na nyota wa tenisi Roger Federer ambaye anakunja kitita cha paundi milioni 34.2 kwa mwaka wakati mcheza gofu mwingine Phil Mickelson yuko katika nafasi ya sita akipokea kitita cha paundi milioni 31.7 kwa mwaka. Nahodha wa zamani wa Uingereza ambaye kwasasa anacheza katika klabu ya Paris Saint-Germain yuko katika nafasi ya saba akikunja kitita cha paundi milioni 30.8 kwa mwaka na anafuatiwa na mchezaji bora wa dunia mara nne Lionel Messi ambaye yuko katika nafasi ya nane kwa kupokea kiasi cha paundi milioni 30. Dereva nyota wa mbio za magari ya langalanga Lewis Hamilton anashika nafasi ya tisa akijikusanyia kitita cha paundi milioni 30 na kumi bora inafungwa na bondia nyota wa uzito wa juu Floyd Mayweather anayekunja kitita cha paundi milioni 29.1 kwa mwaka.

WILSHERE NI MUHIMU ZAIDI KATIKA TIMU YA WAKUBWA - PEARCE.

KOCHA wa timu ya taifa ya vijana chini ya miaka 21 ya Uingereza, Stuart Pearce amedai kuwa kiungo nyota wa Arsenal, Jack Wilshere ana umuhimu zaidi katika timu ya wakubwa kuliko ya vijana. Pearce alithibitisha kuwa Wilshere hatakuwepo katika kikosi cha nchi hiyo kitakachoshiriki michuano ya Ulaya baadae mwaka huu lakini anategemea michuano hiyo itakuwa muhimu zaidi kwa Alex Oxlade-Chamberlain. Kulikuwa na tetesi kuwa Wilshere angejumuishwa katika kikosi cha vijana lakini tetesi zilikanushwa na Pearce ambaye akiri mchezaji huyo ni muhimu zaidi katika kikosi cha wakubwa ambacho kinanolewa na Roy Hodgson. Pearce anaamini kuwa timu ya wakubwa ya nchi hiyo inaweza kupata mafanikio katika michuano mbalimbali kama utamaduni kushinda utajengwa kwa timu za vijana pia kushinda mataji.

FERDINAND ATIMKIA QATAR.

Rio Ferdinand ambaye alijitoa katika kikosi cha Uingereza kitakacheza mechi ya kufuzu michuano ya Kombe la Dunia kutokana na matatizo ya mgongo yanayomsumbua, anatarajiwa kwenda nchini Qatar kufanya kazi ya uchambuzi katika luninga itakayorusha matangazo ya moja kwa moja ya mechi ya Uingereza dhidi San Marino kesho. Beki huyo anayecheza klabu ya Manchester United amekubali kufanya kazi ya uchambuzi katika luninga ya Al Jazeera kwa ajili ya mchezo wa San Marino pamoja na kwamba itakuwa ni safari ya saa 15 mpaka makao makuu ya kituo hicho yaliyopo Doha. Ratiba hiyo ya safari itamsaidia nyota huyo kutatua tatizo lake la mgongo ambalo lilipelekea kujitoa katika kikosi cha Roy Hodgson. Mara baada ya kutua nchini Qatar mapema leo asubuhi Ferdinand aliandika katika ukurasa wa mtandao wake wa kijamii wa twitter kufurahia safari. Uamuzi wa mchezaji huyo kwenda Qatar unaweza kuwakera mashabiki wa soka wa Uingereza pamoja na Chama cha Soka cha nchi hiyo FA.

Wednesday, March 20, 2013

TAARIFA MBALIMBALI KUTOKA TFF LEO.

SERIKALI YARIDHIA MCHAKATO WA UCHAGUZI TFF
Serikali imekubali mchakato wa uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) uendelee kwa sharti la kuhakikisha haki inatendeka kwa wagombea waliofika mbele ya Kamati ya Rufani ya Uchaguzi. Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mchana, Rais wa TFF, Leodegar Tenga amesema uamuzi huo umefikiwa kwenye kikao kati ya uongozi wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo chini ya Waziri Dk. Fenella Mukangara, TFF na Baraza la Michezo la Taifa (BMT). Amesema baada ya maafikiano hayo, TFF italiandikia barua Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) ambalo ndilo lililosimamisha mchakato huo ili litume ujumbe wake kwa ajili ya kusikiliza malalamiko ya wagombea walioenguliwa. Rais Tenga ambaye ameishukuru Serikali kwa kuruhusu mchakato huo uendelee, pia ameahidi kuwa uchaguzi wa TFF utafanyika kabla ya Mei 25 mwaka huu kama walivyokubaliana na Serikali, na kuwa haki si tu itatendeka bali ionekane imetendeka. “Serikali imetuelekeza uchaguzi ufanyike kabla ya Mei 25. Tumewaambia kwetu huko ni mbali. FIFA wakija hata kesho wakituambia endeleeni sisi tuko tayari. Hesabu zetu ziko tayari, makabrasha yote yako tayari yanasubiri mkutano tu. Labda itakuwa kutoa muda tu kwa wajumbe walioko mbali waweze kujiandaa, maana wajumbe huwezi kuwaita ghafla,” amesema. Amesisitiza kuwa TFF ilishapanga tarehe ya uchaguzi, lakini ukasimamishwa na FIFA baada ya baadhi ya walioenguliwa kulalamika huko. Hivyo maneno kuwa TFF hawataki uchaguzi kwa sababu wanataka kuendelea kubaki madarakani haya maana hata kidogo. Hivyo amewataka wagombea wote waliofika kwenye Kamati ya Rufani ya Uchaguzi na wakaendelea kujiandaa vizuri, kwani FIFA watakapofika watawasikiliza wao na vyombo vilivyowaengua. Pia amesema TFF ina heshimu Serikali na itaendelea kufanya hivyo, lakini vilevile lazima iheshimu FIFA sababu iko kwenye mpira wa miguu, na FIFA ndiyo wasimamizi wa mchezo huo duniani. Amewakumbusha wanachama wa TFF, hasa wajumbe wa Mkutano Mkuu kufahamu kuwa TFF ina katiba, lakini ni lazima pia wafahamu kwanini kuna FIFA. Rais Tenga amewahadharisha watu wanaopitapita mikoani kuomba saini za wajumbe ili kuita Mkutano Mkuu wa dharura wakati wanajua mkutano ulishaitishwa, lakini ukasimamishwa na FIFA. Jambo hilo kikatiba ni kosa.

RAIS TENGA AIPONGEZA AZAM KOMBE LA SHIRIKISHO
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga ameipongeza klabu ya Azam kwa ushindi wa mabao 2-1 ilioupata timu yake katika mechi ya raundi ya kwanza ya michuano ya Kombe la Shirikisho. Mechi hiyo dhidi ya Barrack Young Controllers II ilichezwa jijini Monrovia, matokeo ambayo yanaweka Azam katika nafasi nzuri ya kusonga mbele baada ya mchezo wa marudiano utakaofanyika wikiendi ya Aprili 6 au 7 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Amesema Azam imefanya jambo kubwa, kwani kushinda ugenini hasa katika nchi za Afrika Magharibi si jambo dogo, hivyo Watanzania waendelee kuiunga mkono na anaitakia kila la kheri katika mashindano hayo.

TOURE MGUU NJE MGUU NDANI CITY.

KIUNGO nyota wa klabu ya Manchester City Yaya Toure huenda akaondoka klabuni hapo baada ya klabu hiyo kukaa kimya juu ya mazungumzo ya mkataba mpya. Mkataba wa kiungo huyo ambao unamuwezesha kulipwa kiasi cha paundi 220,000 kwa wiki unafikia kikomo 2015 lakini wakala wake anataka klabu hiyo kumpatia mkataba mpya ifikapo Jumamosi na kama wasipofanya hivyo ataanza mazungumzo na vilabu vingine. Toure mwenye umri wa miaka 29 ameripotiwa kujisikia haitajiki klabuni hapo kutokana na klabu hiyo kushindwa kufanya mazungumzo juu ya mkataba mpya katika kipindi cha miezi sita iliyopita. Wakala huyo Dimitri Seluk hadhani kama nyota huyo atabakia klabuni hapo lakini kama atasaini mkataba mpya ndani ya siku nne zijazo anaweza kubakia.

FA KUMPA UBALOZI OWEN.

CHAMA cha Soka nchini Uingereza-FA kipo katika mazungumzo juu ya uwezekano wa mshambuliaji wa zamani wa kimataifa wa nchi hiyo Michael Owen kuwa balozi wa heshima wa chama hicho. Owen ambaye anacheza katika klabu ya Stoke City alitangaza kustaafu soka la kulipwa mwishoni mwa msimu huu baada ya kudumu kwa kipindi cha miaka zaidi ya 16. Lakini Mkurugenzi Mtendaji wa FA Adrian Bevington alibainisha kuwa chama hicho kina nia ya kuendelea kufanya kazi na Owen mwenye umri wa miaka 33 ambaye aliifungia nchi hiyo mabao 40 katika mechi 89 alizocheza. Bevington amesema Owen siku zote amekuwa akijitolea kwa nguvu zake zote wakati akiwa katika majukumu na timu ya taifa ya Uingereza kwa kucheza kwa kiwango cha juu na kufunga mabao muhimu katika michuano mikubwa. Hivyo wanadhani kwa uzoefu wake alioupata katika kipindi alichocheza soka anaweza kuutumia kwa wachezaji wanaochipukia wa nchi hiyo akiwa kama balozi.