Sunday, May 19, 2013

NITABAKI MANCHESTER CITY - NASRI.

KIUNGO nyota wa klabu ya Manchester City, Samir Nasri amesisitiza kuwa atabakia katika timu hiyo msimu ujao baada ya kukanusha taarifa za kufanya mazungumzo na klabu ya Paris Saint-Germain. Kiungo huyo amekuwa na msimu usio wa kuridhisha mwaka huu ambapo amefunga mabao mawili pekee katika mechi 27 alizochezea klabu hiyo msimu huu. Kiwango cha chini alichoonyesha msimu huu kilipodwa vikali na kocha aliyeondoka Roberto Mancini mapema masimu huu hivyo kuzusha tetesi kuwa nyota huyo ataondoka mwishoni mwa msimu huku klabu za Monaco na PSG zikitajwa kuwa ndio atakapokwenda. Lakini mwenyewe amekanusha uvumi huo na kudai kuwa hakuna yoyote aliyewasiliana nae hivyo atabakia jijini Manchester kwa ajili ya msimu ujao.

ROONEY KUWAKOSA WEST BROMWICH.

MSHAMBULIAJI nyota wa klabu ya Manchester United, Wayne Rooney hatasafiri na kikosi cha timu hiyo kwa ajili ya mchezo wa mwisho wa meneja Sir Alex Furguson dhidi ya West Bromwich. Rooney amepewa ruhusa ya kutokwenda huko kwasababu mke wake anategemea kupata mtoto wao wa pili baada kukimbizwa hospitali Jumamosi usiku. Mustakabali wa Rooney Old Traford unatarajiwa kujulikana mapema siku zijazo wakati atakapokutana na meneja mpya wa klabu hiyo msimu ujao David Moyes kwa mazungumzo. Katika siku za karibuni Rooney amekuwa akikosa furaha baada ya kuhisi kama Ferguson hamhitaji tena na kuomba kuondoka mwzi uliopita lakini kocha huyo alimkatalia na kumtaka kuongeza juhudi ili aweze kucheza dakika zote tisini kama anavyopenda. 
Tweet ya mke wa Rooney Coleen akizungumzia ujio wa mtoto wao wa pili.
Lakini Ujio wa Moyes unaweza kubalisha mawazo ya nyota huyo kwasababu ya kufanya nae kazi wakati akiwa kijana mdogo kwenye klabu ya Everton.

VILANOVA KUREJEA NEW YORK KWA MATIBABU YA SARATANI.

MENEJA wa klabu ya Barcelona, Tito Vilanova amebainisha kuwa anatarajia kurejea jijini New York Marekani kwa ajili ya kuendelea na tiba ya matibabu yake ya saratani ya koo. Vilanova alitumia muda wa wiki 10 nchini Marekani mapema mwaka huu kwa ajili ya tiba za mionzi lakini alirejea kuijunga na kikosi chake Aprili. Kocha huyo alipanga kwenda kupata matibabu zaidi mwishoni mwa msimu lakini yeye pamoja na viongozi wa klabu hiyo walikubaliana kuwa anaweza kwenda New York kesho lakini anategemea kurejea Barcelona kwa ajili ya mchezo dhidi ya Espanyol Jumapili ijayo. Katika taarifa iliyotolewa katika mtandao wa klabu hiyo ilithibitisha kuondoka kwa Vilanova kwa kipindi cha wiki moja lakini atarejea Jumapili ijayo kwa ajili ya mchezo dhidi ya Espanyol.

BABA YAKE NEYMAR ASISITIZA MWANAE KUBAKIA BRAZIL.

BABA wa mshambuliaji nyota wa kimataifa wa Brazil na klabu ya Santos, Neymar kwa mara nyingine amesisitiza kuwa mwanae atabakia nchini Brazil mpaka kipindi cha majira ya kiangazi 2014. Kumekuwa na tetesi nyingi kuhusu nyota huyo kutimkia klabu ya Barcelona katika kipindi cha miezi michache ijayo huku kocha wake Tito Vilanova akithibitisha kuwa mazungumzo baina ya pande hizo mbili yamefanyika. Hata hivyo baba yake Neymar amesisitiza kuwa mwanae amepanga kumaliza mkataba wake na Santos akidai kuwa kama Barcelona na Real Madrid zina mpango ya kumsajili nyota huyo basi hawana budi kusogeza mipango yao mwakani. Mzee huyo amesema mipango iliyopo ni kuona mwanae anamaliza mkataba na Santos na kama klabu hiyo ikiamua kumuuza kabla ya mkataba wake kumaliza basi wanapaswa kutoa taarifa kabla ili aweze kuzungumza na mwanae kama yuko tayari kwenda Ulaya.

SIMBA, YANGA WAINGIZA MILIONI 500.

Pambalo la watani wa jadi Simba na Yanga la Ligi Kuu ya Vodacom lililochezwa jana (Mei 18 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kumalizika kwa mabingwa wapya Yanga kushinda mabao 2-0 limeingiza sh. 500,390,000. Mechi hiyo namba 180 ambayo ilikuwa kati ya saba la kuhitimisha ligi hiyo msimu wa 2012/2013 ilishuhudiwa na watazamaji 57,406 waliokata tiketi kwa viingilio vya sh. 5,000, sh. 7,000, sh. 10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000. Kila klabu imepata mgawo wa sh. 123,970,927.45 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 76,330,677.97. Kiingilio cha sh. 5,000 ndicho kilichovutia watazamaji wengi ambapo waliokata tiketi hizo walikuwa 19,039 na kuingiza sh. 95,195,000 wakati kile cha sh. 7,000 kiliingiza watazamaji 17,647 na kupatikana sh. 123,515,000. Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 63,036,064.81, tiketi sh. 3,818,890, gharama za mechi sh. 37,821,638.88, Kamati ya Ligi sh. 37,821,638.88, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 18,910,819.44 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 14,708,415.12.

Saturday, May 18, 2013

TUTAZUNGUMZIA MKATABA MPYA WA LOEW BAADA YA KUFUZU - BIERHOFF

MENEJA mkuu wa timu ya taifa ya Ujerumani, Oliver Bierhoff amesema mazungumzo kuhusu kumuongeza mkataba kocha wa timu hiyo Joachim Loew yataanza mapema timu hiyo itakapofuzu michuano ya Kombe la Dunia 2014. Bierhoff alikaririwa na gazeti la Bild akisema kwamba watakaa pamoja na rais wa Shirikisho la Soka la Ujerumani-DFB Wolfgang Niersbach na katibu mkuu Helmut Sandrock mapema timu itakapokuwa imefuzu ili kuangalia uwezekano wa kumuongeza mkataba Loew. Mkataba wa Loew ambaye ameanza kuinoa Ujerumani toka mwaka 2006 na wasaidizi wake Hansi Flick na Andreas Koepke unamalizika baada ya michuano ya Kombe la Dunia 2014. Kwasasa Ujerumani ndio wanaoongoza kundi lao na kama mambo yakienda vyema kikosi hicho cha Loew kinaweza kikakata tiketi ya kushiriki michuano ya Kombe la Dunia Septemba mwaka huu. 

FERGUSON AIPONDA CITY KUMTIMUA MANCINI.

MENEJA wa klabu ya Manchester United, Sir Alex Ferguson amekosoa uamuzi wa majirani zao klabu ya Manchester City kumtimua kocha wake Roberto Mancini. Mancini alitimuliwa City mapema Jumatatu iliyopita baada ya kuinoa klabu hiyo kwa kipindi cha miaka mitatu na nusu ambayo ameiletea klabu hiyo mataji matatu. Lakini Ferguson ambaye astaafu rasmi baada ya mchezo wa mwisho wa ligi dhidi ya West Bromwich Albion kesho amesema ameshangazwa na uamuzi wa klabu hiyo kumtimua hasimu wake huyo. Ferguson amesema ni jambo la kushangaza timu kumtimua kocha ambaye ameshinda mataji makubwa ndani ya kipindi kifupi na timu yake kumaliza katika mbili za juu lakini alirekebisha kauli yake na kudai kuwa wamiliki wa timu wa siku hizo ndivyo walivyo. Amesema wamiliki wa siku hizo wanahitaji mafanikio ya haraka haraka hivyo wanashindwa kumpa nafasi kocha kujenga timu nzuri ya ushindani.